Hello! Karibu HASCAVELA

Muonekano wa Giza:

Msaada

High School - Episode 03

Kila siku ugumu ulizidi, nilikuwa nikitukanwa kila sehemu niliyokuwa napita na marafiki zake Candy nilichekwa bila sababu, huku nikiendelea kupata adhabu.
Siku moja niliitwa na mwalimu Maloya ofisini kwake niliogopa hata kwenda ingawa sikuwa na jinsi, nilipofika alinikaribisha kwa tabasamu pana lililofanya uzuri wake uzidi kuonekana zaidi.
“Karibu Cathe, karibu ukae.”
Nilikaa kwenye kiti.
“Cathe unajua wewe ni msichana mzuri sana sijaona msichana mzuri kama wewe hapa shuleni, naomba unisaidie kitu kimoja.”
Aliongea, nilishikwa na bumbuwazi lisilo na kifani.
“Nikusaidie nini tena mwalimu, mimi nina uwezo wa kukusaidia kitu gani?”
“Aaaaa usiwe na haraka Cathe nisikilize kwa umakini.”
Aliongea.
Alisimama kutoka kwenye kiti chake akazunguka meza iliyokuwa katikati yetu hadi alipofikia kwenye kiti ambacho nilikuwa nimeketi akanishika begani.
“Cathe nakuhitaji.”
Alisema.
“Aaaaaa hapana mwalimu.”
Niliongea nikiutoa mkono wake.
“Sitaki.”
“Cathe embu nionee huruma mwenzio nakuhitaji sana.”
Alinichefua nilitamani kumwambia kuhusu yeye na Candy lakini nilisita nikaamua kunyamaza kimya.
“Hapana mwalimu ninakuheshimu sana naomba heshima hii iendelee kati yangu mimi na wewe, siwezi naomba uniache.”
Niliongea kwa kujiamni na kisha kutoka nje.

Nikarejea bwenini, sikuweza kuendelea na vipindi vya siku hiyo, nikajifungia mlango nikaanza kulia.
Nikajuta kujua kwangu mahusiano kati ya Candy na Martin na kati Candy na Maloya.
Nilijiona nimejisababishia matatizo makubwa sana kitu ambacho sikujua ni kwamba kuna matatizo makubwa mbele yangu zaidi ya hayo yaliyokuwa yakinikabili, katika maisha yangu yote niliilaumu high school imenibadilisha maisha yangu sana na kunifanya kuwa kiumbe mwenye roho ya utofauti.
Nilianza kukosa raha, maisha ya shule yakawa magumu sana kila nilipopita Candy na kundi lake walikuwa wakinisimanga, matusi, dharau, kusemwa vibaya ikawa kawaida kwangu.
Nilibadili ratiba ili kumkwepa Candy nilichelewa sana kulala na kuwahi sana kuamka, siku nzima ningeweza kukaa darasani.
Maloya pia alinisumbua mara kwa mara alinipa vitisho nilishindwa kumkubali ilionekana kama ni tabia yake kutembea na wasichana wa pale shuleni na kuwapa mimba na kisha kuwatoa alinifanya nizidi kumchukia sana.
Martin naye alikuwa akinipa wakati mgumu sana kadri siku zilivyozidi kuendelea alizidi kukosa amani na furaha hakua Martin niliye mzoea, alikonda sana, kiwango chake cha kusoma kilipungua, alikuwa aonekani darasani mara kwa mara ilibidi walimu waanze kufatilia maendeleo yake.
Kwa upande wangu ufaulu wangu ulishuka pia mwalimu mkuu aliingiwa na wasi wasi alimwagiza matron afatalie kwa ukaribu sana maendeleo yangu ili kujua ni nini tatizo.

Siku moja niliitwa ofisini kwa walimu, jopo zima la walimu lilikuwa mbele yangu walinitazama kwa dharau sana sikuwa najua tatizo ni nini walikuwa kimya tu huku wakinong’onanong’ona.
Mwalimu Maloya alikuwa akionekana akiwa na ghadhabu kuzidi ya walimu wenzie wote.
Nilisimama mbele yao walikuwa wakinitazama bila kusema lolote nilikuwa nimesimama mithili ya mnazi kando ya bahari, nikisukumwa na upepo wa kifikra zisizoleta majibu yoyote.
Mara martin aliingia akiwa na sura ya kukosa tumaini nilijua mambo yameharibika lakini nilishindwa kuelewa ni nini vikao vyote vya kinidhamu lazima Martin awepo kama raisi.
Moja kwa moja nilijua Maloya amenizushia jambo, niliishiwa nguvu nilibaki nikitetemeka na ningeweza kuanguka wakati wowote.
Martin alielezwa asimame pembeni yangu nilishindwa kuelewa maana yake nini kama nimefanya kosa hili peke yangu Martini alitakiwa akae pamoja na walimu kwa nini asimame na mimi hapa, sikunyanyua macho yangu kumtazama Martin nilibaki nimejiinamia mithiri ya mtuhumiwa akisubiri akisubiri hukumu yake baada ya kuthibitishwa kuwa ametenda kosa.
Wapendanao hao sauti kali ya mkuu wa shule mwalimu Maige ilitasua ngoma ya masikio yangu niliishiwa nguvu nikataka kuporomoka.
Martin alinidaka akabaki amenishikilia sikuwa na nguvu ya kuweza kuendelea kusimama nguvu zilikuwa zikiniisha kwa kasi nilipumua kwa shida sana, kitendo cha Martin kunidaka na kunishikilia vile kama amenikumbatia kiupande mkono mmoja ameuweka kiunoni na mwingine amenishikilia bega la kulia kutoka kushoto kwangu alipokuwa amesimama kilitosha kuwafanya walimu wathibitishe uhusiano wetu usiokuwepo.
Machozi ya kukata tamaa yalinitoka.
“Ni nini hii lakini?”
Nilijiuliza tu.
Uchunguzi uliofanywa na baadhi ya walimu juu ya sababu ya kushuka kwa kiwango cha ufaulu wetu mimi na Martin ulileta majibu kuwa tuna uhusiano wa kimapenzi, jambo lisilokuwa na ukweli wowote.
“Sasa cha ajabu nini kinachokushangaza wewe ni nini au kujua kwamba tumeufahamu uhusiano wenu ndio kinachokushangaza zimia kabisa alafu tuone kama kuna kinachobadilika, mtoto Malaya sana wewe umekuja juzi tu umeshaanza mambo ya ajabu ona sasa unavyomshusha mwenzako kimaendeleo Martin hakuwa akifeli hivi.”
Kauli za kejeli ziliwatoka mfululizo walimu hasa wa kike nilisemwa kwa maneno yote mabaya yanayopatikana katika dunia.
Maloya alikuwa na ghadhabu sana hakika alinisema sana.
Nilibaki nikibubujikwa na machozi sielewi hatima yangu walisema sana.
Martin alibaki amenishikilia.

Mwishowe waliamuliwa apigiwe simu baba yangu na kuelezwa, baba alipigiwa simu akaelezwa mbele yangu huku simu ikiwa imewekewa mfumo wa sauti mvumo.
Nilishangaa utulivu wa baba na aliongea kiupole sana haikuwa kawaida nilimjua baba yangu vizuri.
“Cathe hakuwa na tabia hizo ni mambo tu ya ujanani muwaonye waendelee na masomo yao wamalize wafaulu kwa maana hiyo ndio lengo la kuwaleta watoto wetu shuleni na ni lengo lenu sio muwafukuze mtaua ndoto zao muwaache wasome wamalize mimi kama mzazi mzazi wake naomba hivyo.”
Aliongea kwa utulivu, nilibaki nimeshangaa sikutaka kuamini kama huyu ni baba yangu Mzee Kindamba.
Mkuu wa shule aliongea na baba na kumwambia kuwa nimekuelewa na tumewasamehe watoto hawa na hatuta wafukuza shule tutawapa adhabu na kisha waendelee na masomo yao.
Nilivuta pumzi ya shukurani kwa sababu jinsi navyomjua baba ageweza kuwaambia walimu wanifukuze shule nirudi nikakae nyumbani hakupenda nifanye ujinga wowote.
Ilijadiliwa kuwa Martin aondolewe cheo kama raisi wa shule baadhi ya walimu walipinga kwasababu utendaji kazi wake ulikuwa uko juu na pia shule ingeendeshwa bila kuwa na kiongozi mkuu wa serikali ya wanafunzi hivyo ingeleta shida katika uwasilishwaji wa matatizo ya wanafunzi katika uongozi wa shule hivyo alionywa endapo tatizo hili likijirudia tena hatua za kinidhmu zitachukuliwa dhidi yake.
Martin alisimama bila kuongea chochote akiwa amenishikilia na sura yake aliyokosa matumaini akiwa ameielekeza kwa chini. Nililaumu nafsi yangu kuwa chanzo cha matatizo ya Martin.

Tulitolewa ofisini hadi katika eneo la mkutaniko.
Kengele iligongwa wanafunzi wote walisogea pale.
Mkuu wa shule alisimama na kisha kuongea kwa sauti kali.
“Mmekuja hapa shuleni kwa ajili ya kusoma mnapaswa mfuate kilichowaleta hapa sisi tupo hapa kuwasaidia kutimiza ndoto zenu kila kitu kina wakati wake, mambo mengine yote mtayakuta.
Fanyeni kilichowaleta hapa na mwachane na mambo mengine yote.”

Kisha mkuu wa shule aliondoka akiwa amejawa hasira sana.
Mwalimu wa nidhamu alijongea mbele na kisha kuueleza umma wa wanafunzi makosa yetu mimi na Martin, makosa yasiyo na ukweli wowote.
Wapo walionicheka wapo walionikebei na wapo wachache waliohuzunika kwa ajili yetu.
“Adhabu yao tutawachapa mbele yenu ili iwe fundisho kwenu na kisha watapewa wiki mbili za kufyeka manyasi yaliyopo nyuma ya shule na baada ya hapo watakuwa mawesamehewa.
Na nilazima kwa wao kuingia darasani vipindi vyote bila kukosa na ndani ya wiki mbili lazima wawe wamemaliza kufanya kazi waliyopewa”\n Aliongea mwalimu wa nidhamu na kisha kuanza kutuchapa mimi na Martin.
Lilikuwa ni tukio la aibu sana kuwahi kutokea katika maisha yangu kuadhibiwa mbele ya wanafunzi wenzangu kwa kosa kama hilo, niliumia sana moyoni.
Tulichapwa fimbo nyingi tu mimi na Martin na kisha wanafunzi wakaruhusiwa kurejea darasani huku wakiongea mambo mbalimbali kuhusiana na tukio hilo.

Nilianza adhabu yangu ingawa kiunyonge zaidi kila mara nilipokuwa eneo la adhabu nilikuwa nikilia sana, sikutamani kukutana tena na Martini ingawa sikuwa na jinsi kuonana nae wakati wa vipindi darsani, mara zote sikupenda kumwangalia.

Siku ya tatu ya adhabu yangu niliitwa na mwalimu ofisini kwake alikuwa ni mwalimu wa michezo, sir Benson.
Nilipofika aliniambia kuna simu kutoka kwa mama yangu.
Alimpigia simu mama na kisha nikaongea nae.
“Mwanangu Cathe uhali gani.”
Aliongea mama kwa sauti ya upole.

“Mama mimi mzima, shikamoo mama.”
Nilimwamkia.
“Marhaba mwanangu nimekukumbuka sana.”
“Mimi pia mama.”
Nilimjibu.
“Cathe nataka nikwambie kitu mwanangu.”
“Ndio mama nasikia.”
Nilisema.
“Natamani sana utimize ndoto zako ufike pale ulipokuwa unatamani kufika mwanangu, usiwe na haraka na haya mambo usikimbilie kula pilau kabla haijaiva unakosa utamu wake ni vibaya.”
Aliongea kwa huzuni.
“Naelewa mama ni makosa tu mi binadamu nakuahidi kwamba hayatatokea tena.”
Nilisema.
“Usijali mwanagu yote ya dunia siku moja utafika unakotaka kufika, hiyo itakuwa furaha yako.”
Alisema kwa upole nakutakia.
“Kila la kheri mwanangu tutaonana mungu akipenda.”
Alisema na kukata simu.
Nilijawa na furaha yenye uchungu nilifurahi sana kuongea na mama yangu lakini nilisikitika kwa maneno aliyoniambia na kwa upole aliouonesha niliondoka ofisini nikiwa na mawazo mengi.
“Mama yangu na baba yangu siku hizi wamebadilika sana natamani kuwaona tena.”
Nilirejea bwenini.
Zilipita siku kama tano nilipoitwa tena ofisini kwa mwalimu.
Mwalimu alinitazama kwa jicho la uchungu sana.
“Cathe.”
Mwisho aliamua kuniita.
“Abee mwalimu.”
“Yote ni mambo ya dunia kuna siku utayavuka na kuwa na furaha tena.”
Aliniambia.
“Najua mwalimu.”
Nilijua alikuwa akihudhunika sana kutokana na matatizo yaliyokuwa yakinikumba hapo shuleni.
“Kuna simu yako.”
Aliongea huku akishusha pumzi.
Nilipokea.
“Mwanagu cathe.”
Aliongea baba kwa sauti ya upole kuliko ilivyokawaida.
“Bee Baba shikamoo.”
“Marhaba ujambo.”
“Sijambo.”
Sauti yake ilizidi kufifia kila alipokuwa akiongea.
“Unaendeleaje mwanangu.”
“Naendelea vizuri.”
Nilisema.
“Mwanangu Cathe.”
Aliiniita.
“Abee baba.”
Alinyamaza kimya nilishindwa kuelewa mapigo yangu ya moyo yalianza kwenda kasi, nilishindwa kujua tatizo ni nini.
“Baba.”
Niliiita.
“Eee mwanangu.”
Aliongea kwa sauti ya kilio.
“Kuna nini?”
Nilimuuliza.
“Mwanangu.”
Aliniita.
“Mama yako mpenzi amefariki dunia.”
Aliongea baba kwa sauti iliyochanganyika na kilio.
“Say whaaat?”
Niliongea kwa mshituko sana.
“Ni hivyo mwanangu, kazi ya mola haina makosa.”
Machozi yalinichuruzika mfululizo huku mdomo ukitetemeka nilishindwa kuongea neno lolote.
“Cathe.”
Baba aliinita kwa utulivu.
Nilishindwa kuendelea.
Aliongea.
“Pamoja na hayo yote nasikitika kukwambia kwamba hutoweza kuhudhuria mazishi yake kwa maana anazikwa leo.”
Maneno hayo yalinishingaza nilipata ujasiri wa kuongea.
“Baba kwanini sipaswi kuudhuria mazishi ya mama yangu, ina maanisha mama amefariki na siwezi kuona sura yake ya mwisho kwanini sikupewa taarifa mapema baba kwanini lakini?”
Niliongea kwa sauti kubwa ya kilio.
“Hapana mwanangu hatuna jinsi mama yako hawezi kuendelea kukaa tena naomba unielewe endelea kusoma utakuja wakati wa arobaini yake.”
Aliongea baba.
Niliangua kilio kikubwa hatukuweza kusikilizana tena.
Baba alikata simu.
Nililia, niliona duniani niko peke yangu nilihisi nimetengwa mbali na dunia sikuwa sawa na viumbe wengine roho iliniuma kuliko kawaida, sikuwahi kuhisi maumivu makali moyoni kama nilivyoyahisi kwa wakati huo, nililia sana sikuwa na nguvu ya kunyanyuka.
Mwalimu alini onea huruma alininyanyua akanikokota kuelekea bwenini wakati tuko njiani tulipishana na Martin.
Martin alikuwa amekonda sana nilimtazama huku nikilia kwa sauti mwalimu aliniongoza mpaka bwenini akaanza kunifariji kwa maneno mazuri.
“Hii ni njia ya kila mmoja wetu kila mtu atapita, kila nafsi itaonja mauti jipe moyo Cathe.”
Nililia sikuwa namsikiliza alikuwa anaongea nini wala sikutamani kusikia alichokuwa akiongea.
“Kwanini baba asinipe taarifa na kuhudhuria msiba mapema kwanini?”
Nililia huku nikiwaza hayo yote, nilishindwa kupata majibu.

Sehemu 2 Sehemu 4
0
0