Hello! Karibu HASCAVELA

Muonekano wa Giza:

Msaada

Formula - Episode 01

“We Lucy unajifanya humjui wewe?”
“Lucy yupi?”
“Lucy humjui huyo anakaa hapo jirani yetu hapo nyumba ya tatu kutoka hapa, kwa mama Sakina!”
“Aaaanh, si huyo ambaye anasoma form four?”
Walionekana mtu na Mama yake wakibishana.
“Huyohuyo.”
“Eenhe kafanyeje?”
“Kaenda kuhangaikahangaika huko limempata la kumpata, nyie mabinti wa siku hizi sijui mnatafuta nini?! Kaenda kuzururazurura kuhangaikahangaika shule hataki wazazi hawasikilizi kiburi kimemjaa aya sasa kaenda kuokota mimba na hata baba mtoto kamkataa yupo tu hapo analialia. Yani mama yake amekasirika ningekuwa mimi ningemvunja miguu yake mpumbavu yule.”
Sitti alionekana kuogopa alishindwa hata cha kuongea.
“Yani sikia nikuambie kitu Sitti zunguka uzungukavyo hangaika uhangaikavyo usije ukaniletea mimba hapa kwangu yani nitakutafuna, nitakukula mbichimbichi.”
Aliendelea kuongea Mama yule.
Sio siri Sitti aliogopeshwa sana na yale maneno.
“Mmmh mama hebu nisimulie vizuri ilikuwaje.”
“Nikusimulie nini usichokijua...?”
“Mwanangu usidanganyike soma, yani huyu ndiyo ameshachezea maisha yake, kabinti kadogo halafu ndiyo alikuwa form four.
Aya shule kakosa mwanaume kamuacha na mimba juu amebakia analialia.
Mwanangu soma maisha magumu soma.
Yani soma mpaka mwisho mpaka madarasa yaseme basi imetosha soma mpaka mwisho mwanangu elimu ndiyo ufunguo wa maisha usiache elimu soma mama.”

Mama yule aliendelea kumsisitiza binti yake.

Sitti aliendelea kuosha vyombo huku akitafakari maneno ambayo alikuwa ameambiwa na mama yake kwa upande mwingine aliona ni kweli.
“Asa kwa mfano amepewa mimba shule ndiyo anaacha! Halafu na baba wa mtoto amekataa mimba itakuwaje? Ila wanaume hawa wabaya! Wakati huo anamtongoza alikuwa anampa vihelahela huko saa hizi amebeba mimba anamkimbia looh masikini Lucy ameshachezea maisha yake.”
Sitti aliendelea kujiwazia mwenyewe.
Hata usiku ulipofika mama huyo alimuweka kitako binti yake.
“Mwanangu Sitti nimekuita tena mara nyingine angalia dada zako wamesoma wameolewa na wanaishi vizuri.
Hawanitegemei mimi maisha yao yanaendelea vizuri kabisaa na wana watoto na familia zao.
Usikimbilie hayo mambo utayakuta tu wanaume hawaishi hawaendi kokote wapo.
Kwahiyo cha msingi mwanangu soma usipuuze elimu hata vitabu vya dini vimeandika usimuache elimu aende zake.
Sitti soma mama.
Hamna kitu chochote ninachoweza kukupa mimi mama yako zaidi ya elimu sina hela sina nini, elimu ndiyo kitu pekee unachotakiwa kukizingatia kwa sasa utasoma utamaliza utapata mwanaume mzuri atakuoa utapata kazi nzuri utafanya, utazaa watoto hata hawatateseka lakini kukimbilia hawa vijana wa saa hizi vijana wenyewe wananuka hata kuoga vizuri hawajui wachafu na hizi nywele zao wanazoziacha kichwani ni chafu na zina na chawa juu achana nao mama soma sawa.”

“Ndiyo Mama.”
Aliitikia Sitti.

Maneno ya Mama yake yalionekana kumuingia.
Wakati akiendelea kutafakari hodi ilibishwa.
Baba yake na Sitti alikuwa akirudi nyumbani muda huo.
Mama Sitti alimkaribisha mume wake.
“Vipi kuna kikao hapa?”
Aliuliza Baba Sitti.
“Haaah niko namhusia huyu binti maana kilichotokea hapo mtaa wa pili mume wangu umekisikia?”
“Nini tena?!”
Aliongea Baba Sitti huku akikaa chini.
“Si huyu Lucy amepata mimba.”
“Lucy yupi?”
“Huyu Lucy anayekaa hapo kwa Mama Sakina yule mdada aliyekuwa anasoma form four.”
“Eeenh ya nani tena?”
“Hata anajua basi kijana mwenyewe nasikia amekataa mimba mama yake nae amekasirika ni analia tu jamani yani nyie mabinti mtuonee huruma si wazazi wenu tunahangaika kwaajili yenu jamani msije mkatukata maini na kutudhalilisha.”
Aliongea Mama Sitti.
“Sitti unamsikia mama yako soma sawa.”
“Ndiyo Baba.”

Mama Sitti aliandaa chakula akisaidiwa na Sitti na baada ya kumaliza chakula cha usiku kila mtu alielekea sehemu yake ya kulala.
Sitti bado alikuwa akitafakari.
“Mmmh hapa inabidi nisome tu kwa kweli sitaki kuleta aibu kwenye familia yetu kama alivyofanya Lucy.”

Baba Sitti, bwana Isaka alikuwa ni mwalimu wa shule ya sekondari wakati mkewe alikuwa nae ni mwalimu wa shule ya chekechea ambayo ilikuwa hapo mtaani kwao.
Maisha yao hayakuwa mabaya, Baba Sitti na Mama Sitti walikuwa na watoto watatu ambao ni Elizabeth na Neema.
Elizabeth na Neema tayari walikwisha maliza masomo yao na walikuwa wameolewa na wana familia zao na walikuwa wakiishi sehemu nyingine hapo nyumbani alibakia Mama Sitti, Sitti na Baba yake na Sitti na mtoto wa mjomba wake aitwaye Rozina ambaye tayari alikuwa amemaliza kidato cha nne huku matokeo yake yakimzuia kuendelea na kidato cha tano.
Alikuwa hapo akisubiri kujiunga na chuo kwa ajili ya kujiendeleza kielimu.

Sitti aliamua kusoma kwa bidii sana kila siku alipotoka shuleni mama yake alikuwa akimhusia kuhusu swala la kusoma na kuachana na vijana.
Kila mkaka ambaye alikuwa akimtongoza Sitti alimuona ni adui wa maendeleo yake sio siri alichukizwa sana alibadilisha na njia kabisa endapo ikitokea mmoja kati ya vijana walikuwepo hapo mtaani wakimsumbua.
Sitti mwenyewe alikuwa ni binti mrembo tu na vijana wengi wengi walikuwa wakimsumbua hata hivyo hakutaka hata kuongea nao aliwakwepa na kuamua kuishikilia elimu.

Alipofika kidato cha pili mara baada ya kumaliza mtihani baba yake alimuita.
“Unataka kusomea nini mwanangu?”
“Baba mimi nataka kusomea masomo ya biashara.”
“Nini?!”
Mama yake Sitti alimuambia.
“Kwani masomo ya sayansi yanakushinda nini?”
“Hapana mama lakini mimi napenda sana masomo ya biashara.”
Mama Sitti alikaa kimya.
“Yani wewe utaenda tu kuwa kama Lucy yani lazima uje ututie aibu umeacha kuchagua masomo mazuri ya sayansi unaenda kuchagua masomo ya biashara una akili kweli wewe.”
“Mama bwana mimi siyo siri nitachukua masomo ya biashara.”
“Biashara siku hizi haina maana.”
“Hebu kwanza Mama Sitti muche mtoto basi aongee.”
Aliingilia kati Baba Sitti.
“Ngoja kwanza subiri nitafuatilia sana hiyo mambo halafu nitakuja nikushauri.”
Baba yake aliongea.
“Ok.”

Kesho yake tena Sitti aliitwa.
“Mwanangu masomo ya biashara siyo mabaya lakini hayo mambo mpaka uwe na connection cha msingi wewe chukua masomo ya sayansi ukifaulu vizuri unaenda kusomea unesi, udaktari hizi ajira ziko njenje serikali inaajiri kila siku, walimu serikali inaajiri kila siku kwahiyo cha msingi usisome masomo ya biashara nenda kasome masomo ya sayansi.”
“Lakini mama mimi nilikuwa nataka kusoma masomo ya biashara.”
“Yani wewe mtoto ni mbuzi kabisaa… Yani tunahangaika kumpeleka shule huyu mbuzi.”
Mama Sitti alidakia.
Sitti alibakia ameinama tu.
“Wewe ushawahi kuona wapi watu wanasoma biashara, mimi namjua mama Selina kule shuleni hajawahi kwenda shule hata kidogo lakini anafanya biashara zake vizuri, wewe unataka kwenda kusomea biashara ipi hivi unajielewa kweli?!”
Mama mtu alizidi kugomba.
Sitti alijiinamia.
“Sikiliza mwanangu.”
Baba Sitti aliingilia.
“Masomo ya biashara siku hizi hayana mpango bora ukasomee masomo ya sayansi.”
“Lakini Baba mimi katika masomo ambayo nafanya vizuri ni ya biashara masomo ya sayansi sijaweza kuyaweza vizuri kwahiyo itanipa shida sana.”
“Acha shule.”
Mama yake aliingilia.
“Subiri kwanza Mama Sitti.”
“Aache shule kama hawezi, eti mtu unaaenda shule unasema hili somo naliweza na hili somo siliwezi. Acha shule ukae nyumbani tujue moja kwamba shule imekushinda.”
Siyo siri Sitti alikwazika sana lakini hakuwa na namna angefanyeje na wazazi wake wameshasema hivyo.
Alinyanyuka kiupole na kisha kwenda chumbani kwake.
Aliwaza na kuwazua.
“Jamani mimi physics nitaweza kweli jamani, itakuwaje? Sawa liwalo na liwe.”
Aliwaza na kuwazua.

Alijitahidi kusoma hata matokeo ya kidato cha pili yalipotoka alienda kujiunga na darasa la sayansi.
Alipoingia kidato cha tatu ndugu yake Rozina alibambwa akiongea na kijana ambaye alikiri kuwa na mahusiano naye.
Wazazi wa Sitti waliamua kumrudisha kwa baba yake, yaani mjomba wake Sitti kuhofia kuaibishwa na ile ahadi ya kumpeleka chuo ikaishia hapo.
Jambo hili lilimtisha Sitti.
Aliwaza endapo angecheza kidogo basi maisha yake yangeharibika kwa kiasi kikubwa sana.
Alijitahidi kusoma kadri ya uwezo wake ingawa physics ilikuwa ikimuadhibu.
Pamoja na changamoto zote lakini alijitahidi sana kusoma hakutaka kufanya ujinga wa aina yoyote ule.
Alijilinda, alijitunza mpaka alipomaliza kidato cha nne.

“Yani ukifeli Sitti, ukifeli… Nakuozesha kwa kuku haooo… wawili, (huku akionesha kwa vidole viwili.) maana bora nipate kuku nifuge kuku wawili wakija wakazaa napata vifaranga vingi tu wanakuwa wanakuwa baadae nakuwa na kuku wengi, nakula na mayai kuliko kukaa hapa nikakulisha bure na kukuvalisha bure yani nilipe ada miaka minne halafu uje ufeli katafute pa kukaa labda sio hapa. Ukijiona tu umeenda kuangalia matokeo yako ya kidato cha nne ukajiona umefeli usirudi kabisa nyumbani nisione uso wako hapa nisione hizo kongoro zako.”
Mama Sitti alikuwa akimuambia binti yake mara kwa mara.

Siku ya matokeo ilifika Sitti alikuwa amepata daraja la tatu.
Alifurahi sana.
Alirudi nyumbani kwao kwa furaha.
Mama yake alifurahi mno.
Alipiga mayowe mpaka majirani walikuja kuuliza kuna nini kimetokea.
“Mwanangu jamani kafaulu jamani.”
Alikuwa akiongea watu wote waliosogea nyumbani kwao hapo walikuwa wakimpongeza.
Huku Sitti akipewa hongera nyingi mno kiasi alijisikia upekee.
Aliona amechagua fungu jema sana kumsikiliza mama yake tangu zamani.
Aliheshimika mtaa mzima.
“Aanh kasichana kana akili kale kamepasua mitihani yake ya taifa.” Kila mtu alikuwa akimsifia.

Maisha yalienda hatimaye alichaguliwa kujiunga na kidato cha tano kwa mchepuo wa CBG.
Baada ya maandalizi hatimaye alienda shuleni.
Kila mara aliporudi nyumbani watu wengi wa pale mtaani hasa watu wazima walikuwa wakimuuliza kuhusu mambo ya shule.
“Kazana mdogo wangu soma maisha yenyewe ndiyo haya haya bila elimu siku hizi mambo yatakuwa magumu sana, soma usiache elimu.”
Watu walimshauri.
Na yeye Sitti pia aliamini katika elimu.
Alisoma kwa bidii zote ingawa masomo ya sayansi yalikuwa ni magumu sana lakini alijitahidi kusoma kadri ya uwezo wake.
Hatimaye aliweza kumaliza kidato cha sita.
Alirudi nyumbani kwao.
“Eeeh mwanangu hongera sana tumuombe Mungu sasa nako ufaulu vizuri uende chuo jamani ukakamilishe ndoto zako.”
“Sawa mama nashukuru.”
“Unamkumbukaga yule Lucy yule aliyekuwa anakaa pale kwa kina mama Sakina?” “Eeeh namkumbuka.”
“Hivi alijifungua?”
“Eeh alijifungua mtoto mweusiiiii kafanana sijui na baba yake sijui, sijui ndiyo huyo.
Siku hizi anafanya biashara mwenyewe anapikapika vitumbua sijui maandazi.
Looh angekuwa anasoma saa hizi si angekuwa chuoni na yeye sahivi maisha yameshamnyookea, ona sasa saivi hana kazi kazi kutupigia kelele asubuhiasubuhi vitumbuaaaa sijui nini… binti mbaya yulee…”

Aliongea Mama Sitti.
Sitti aliamua kukaa kimya tu.
“Eeenhe mwanangu sasa kwahiyo huko shuleni unategemea nini?”
“Mama tuombe Mungu tu kitakachotokea ndiyo hikohiko.”
“Hebu acha ujinga wewe unatakiwa ufaulu mtaa mzima mimi ndiyo nasifiwa mtoto wangu ndiyo msomi ana akili lazima ufaulu.”
Mama yake aliendelea kumpa maneno.

Mungu naye hakumuacha.
Wakati matokeo yalipotoka alipata daraja la tatu.
Kama kawaida yake Mama Sitti mtaa mzima ulijua.
“Hongera sana mwanangu itabidi nikutafutie zawadi.”
Aliongea mama Sitti huku akichekacheka na kweli alimtafutia Sitti zawadi.
Mpaka wakati huo Sitti aliendelea kushikilia msimamo wake alitaka kumaliza kwanza shule na ndipo aanze kutafuta kuwa na familia.
Alijitunza kwaajili ya mume wake mtarajiwa.
Vijana wengi pale mtaani kwao walikuwa wakisema kuwa Sitti alikuwa anaringa hata mama yake aliposikia alizidi kumpa bichwa mwanae.
“Ndiyo, vijana wabaya wale ndiyo haohao waliompa mimba Lucy wakamuacha eti wanasema unaringa tena uringe zaidi ya hapo uringe, mwanangu msomi umesomaaa eeenh wale sio level zako wale madereva bodaboda watakupa nini wewe msomi unaenda kujiunga na chuo kikuu watakupa nini achana nao.”
Mama Sitti aliendelea kumpa kichwa mwanae.

Muda wa kujiunga na chuo ulipokaribia tafrani ilitokea wakati Sitti alipotoa wazo la kwenda kusomea ualimu kama wazazi wake.
“Hivi Sitti mwanangu mbona lakini unafaulu darasani lakini kwenye maisha huna akili hebu tuangalie sisi wazazi wako wote hapa ni waalimu tumefanya nini cha maana hebu angalia tunafanya nini cha maana wewe unataka uishi kama sisi?
Soma kozi nzuri ambayo itakupa ajira nzuri utapata kazi nzuri itakulipa hela nyingi wewe unataka kusomea ualimu kweli jamani huyu mtoto jamani sijui nilimtoa wapi!”

Sehemu 2
0
0