Nataka Kuzaa - Episode 01 
Ilikuwa ni siku ya Jumatatu, tarehe tano mwezi wa kumi mwaka 2015.
Asubuhi ya saa mbili ilinikuta mimi na familia yangu tukiwa mezani tukipata kifungua kinywa.
Ilikuwa ni asubuhi yenye furaha na bashasha.
Mimi, baba yangu, mama yangu na wadogo zangu wawili mapacha Pink na Pinto tulikuwa tukinywa chai tukiongea mambo mbalimbali.
Ni siku hiyo ambapo hata wadogo zangu hawakutamani kwenda shuleni, wazazi wangu pia hawakwenda kazini hiyo siku.
Yote yalikuwa ni maandalizi ya kunipeleka chuoni ambapo kwa mara kwanza
nilikuwa naingia chuo kikuu cha Dar Es Salaam
kusomea kozi ambayo ilikuwa ni ndoto yangu na ya wazazi wangu, kozi ya udakatari.
Hakika ilikuwa ni siku ya furaha sana.
“Sociolah unajisikiaje mwanangu?”
Mama aliniuliza.
“Mmmh mama sijui hata jinsi gani nikuelezee.”
Niliongea huku nikichekacheka.
“Nimefurahi sana kwasababu ni leo ambayo siku natimiza ndoto zangu na zenu pia, najua jinsi ambavyo mimi najisikia na nyie mnajisikia hivyohivyo.”
Niliongea na kumalizia kwa cheko pana, wote walicheka isipokuwa wadogo zangu ambao walikuwa bize wakichezacheza michezo yao hapo mezani.
Baba yangu Michael Kindamba ambaye alikuwa ni Daktari wa Muhimbili alisema huku akitafuna chakula mdomoni.
“Hamna Sociolah sisi tuna furaha sawa lakini furaha yetu haiwezi kuwa kubwa kuliko furaha yako.”
Mama yangu Anastazia Kindamba ambaye alikuwa ni mhadhili wa chuo kikuu cha Dar Es Salaam kwa masomo ya uchumi alicheka.
“Ni kweli lazima furaha yako imetuzidi ila unajifanya kama hujafurahi vile Sociolah.”
Aliongea na kumalizia kwa kucheka.
Hakika ilikuwa ni siku ya furaha sana kwetu.
Pink na Pinto hawakuwepo mbali hawakutaka kwenda shule hiyo siku waling’ang’ania kuja chuoni kunipeleka kwaajili ya usajili.
Tuliondoka nyumbani kwetu maeneo ya Mbezi beach na kuelekea chuo kikuu cha Dar Es Salaam.
Ndani ya gari nilikaa nyuma na wadogo zangu ambao hawakuishiwa fujo, hakika walikuwa watoto watundu sana,
mara zote nilijaribu kuwaongoza “usifanye hiki, usifanye kile” walikuwa wabishi ingawa walileta furaha sana katika familia yetu.
Mimi na wadogo zangu tumepishana umri mkubwa sana wazazi wangu walisubiri sana kabla ya kuwapata wadogo zangu.
Mimi nina umri wa miaka ishirini na moja na wadogo zangu wana umri wa miaka kumi na moja hivyo tulikuwa tumepishana miaka kumi kati yetu.
Tulifika chuo kikuu cha Dar Es Salaam na kuelekezwa katika ukumbi wa Nkuruma ambapo shughuli za usajili zilikuwa zikifanyika.
Mama yangu alikuwa mfanyakazi wa chuo kikuu cha Dar Es Salaam kwahiyo haikutuwia vigumu sana kufanya usajili.
Niliweza kuchukua fomu ya kujiunga na kisha nikafanya usajili wa bima na pia nikaenda kupiga picha za vitambulisho.
Baada ya hapo nilielekea benki kwaajili ya kulipia ada pamoja na hostel. Nilikuwa nimepangiwa kukaa hostel za mabibo.
Baba yangu hakupenda nikae hostel.
“Mwanangu si uwe unakaa hapa hapa nyumbani nitakupa gari utakuwa unaenda nalo chuoni mimi sipendi ukae mbali na sisi.”
“Mmmh baba itaniwia vigumu sana kama nitakaa hapa nyumbani kwa maana wakati mwingine tutahitaji kuwa na discussion
nitapata shida baba, kila weekend nitakuwepo hapa nyumbani usijali kuhusu mimi alafu saa hizi baba mimi nimeshakua hivyo
siwezi kuendelea kukaa hapa nyumbani kudekadeka tu.”
Niliongea huku nikicheka baba naye alicheka.
Mama alinisapoti.
“Anachokiongea Sociolah ni ukweli muache aende akakae hostel na kila weekend awepo hapa nyumbani.”
Mama aliongea tulikubaliana.
Baada ya kutoka Benki tulienda cafe kula hakika ilikuwa ni furaha sana tulikula katika cafe iliyokuwa inaangaliana na shule ya biashara pale chuo kikuu cha Dar Es Salaam.
Tulirudi Nkuruma kwaajili ya kumalizia Shughuli za usajili.
Nilibaki nimesimama mlangoni pale Nkuruma, baba na mama yangu waliingia ndani kwaajili ya kuangalia
ni nini kilichokuwa kinaendelea.
“Dada… dada….njoo ucheke.”
Pink na Pinto waliniita.
“Hawa watoto wasumbufu kweli wameona nini?”
“Njoo…”
Nilisita kwenda lakini sikuwa na budi kwa vile baba na mama walikuwa ndani ya ukumbi ule na mimi nilikuwa
nimesimama mlangoni nilisogea hatua chache na kisha kuwafikia Pink na Pinto.
“Angalia pale”
Niliangalia lakini sikuona kitu.
“We dada huoni angalia bwana mwenyewe asije akatuona”
Pink aliongea huku akicheka.
Niligeuka na kutazama pale ambapo walikuwa wakinionesha hakika kilikuwa ni kichekesho cha mwaka,
nilishindwa kujizuia kucheka.
Alikuwa ni mkaka ambaye amesimama huku akiwa hana hili wala lile.
Alikuwa akibonyeza simu yake ambayo sikusita kuitambua kwamba ni nokia ya tochi.
Hakika jinsi alivyokuwa amesimama na muonekano wake ilikuwa ni kichekesho tosha, watu wengi walikuwa
wakimuangalia na kucheka.
Alikuwa amevaa tshirt ya light blue iliyopauka, alikuwa amevaa suruali aina ya bwanga
rangi ya kijivu alikuwa amechomekea tshirt yake ndani ya suruali hiyo.
Chini alivaa raba nyekundu, mkononi alikuwa ameshikilia tranka lake na kichwani alikuwa amevaa kofia aina ya pama.
Hakika alionekana kama mkulima aliyekuwa akielekea shambani au mganga wa kienyeji alieamua kuvalia vizuri,
nilishindwa kujizuia nilicheka kisha nikawavuta wadogo zangu kuelekea ndani ya ukumbi, nikawakemea.
“Sio vizuri kumcheka mtu”
“Dada kwani huku mnakujaga na matranka?”
Waliniuliza, nikawaambia.
“Hebu acheni huko muacheni mtoto wa watu mnamcheka mnamcheka nini baadae atakuja kuwa mtu mkubwa
mpaka mtashangaa niliongea”
“Mmmh.”
Waliishia kucheka tu ingawa ilikuwa ni kichekesho lakini sikupenda kuwadharau watu.
Baada ya shughuli za usajili kuisha tulirudi nyumbani tukiwa tumechoka huku tukifurahia safari ile.
Baada ya kuoga tulipata chakula cha jioni kilichoandaliwa vema na mfanyakazi wetu wa ndani aliyekuwa ni
msichana wa makamo tuliyezoea kumuita Linah ingawa jina lake aliitwa Paskalinah.
Baada ya chakula cha jioni tulikaa verandani tukiongea mambo mbali mbali kuhusiana na siku yetu iliyopita.
Pink aliyekuwa akichezea simu ya baba alimgeukia mama na kumuonyesha kitu mama alicheka hadi machozi yakamtoka.
“Nini unacheka mama.”
Baba aliuliza.
“Mwambie Pink akuonyeshe.”
Alijibu huku akifuta machozi.
Pink alimpa simu baba.
“Imetoka wapi hii.”
Baba aliuliza kwa mshangao uliofuatiwa na kicheko.
“Mimi ndo nilipiga.”
Alijibu Pink kwa kiherehere.
“Jamani kuna watu ni vituko.”
Mama alisema.
“Ni nini?”
Niliuliza.
“Si ni yule mkaka wa chuoni niliekuonesha”
Pinto alidakia.
Nilichukia, nikanyanyuka nilipokaa hadi kwa baba aliyekuwa ameshika simu nikaichukua kwa nguvu nikafuta picha zote walizompiga yule kaka.
“Sio vizuri kumbeza na kumcheka mtu kwa muonekano wake hamjui hata katokea
wapi wala anaenda wapi (niliongea kwa hasira) sijapenda, Pink na Pinto acheni hiyo tabia”
Wote walishikwa na butwaa nadhani hawakuamini kama ningeweza kumtetea mkaka yule aliyekuwa
kituko na ambaye sikuwa nikimfahamu hata kidogo.
Sikujali niliirudisha simu kwa baba na kuelekea chumbani kwangu kupumzika sikutaka kuendelea kuwepo hapo.
“Mmemskia dada yenu, siku nyingine msirudie”
Mama aliongea sikujishughulisha kuendelea kusikiliza maongezi yao nilibamiza mlango wa chumba changu.
Unaweza pia kusoma: